CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 6 April 2020

VETA yaendelea kuaminiwa kushona sare za Daladala


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe, amezindua sare mpya za madereva na makondakta wa daladala Jijini Dar es Salaam ambapo Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imepewa tena zabuni ya kuendelea kushona sare hizo.

Kwa mara ya kwanza VETA ilipewa zabuni ya kushona sare hizo mwaka 1998.


Uzinduzi wa sare mpya umetokana na mahitaji na mawazo ya uboreshaji wa sare hizo yaliyotolewa na Chama cha Wamiliki wa Daladala (DARCOBOA) na Umoja wa Wasafirishaji Abiria Jijini Dar es Salaam (UWADAR).


Sare hizo zinajumuisha kaunda suti za rangi ya zambarau na fulana za rangi ya damu ya mzee ambapo utaratibu wa kuvaa utakuwa ni suti kuvaliwa siku za wiki na fulana kwa siku za mwisho wa juma.


Akizungumza wakati wa uzinduzi huo leo tarehe 6 Aprili, 2020 jijini Dar es Salaam, Waziri Kamwelwe amesema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa huduma ya usafiri hasa kwa kuzingatia kuwa zaidi ya asilimia 90 ya wafanyakazi na wafanyabiashara wa Mkoa wa Dar es Salaam, wanategemea usafiri wa umma kufika kwenye maeneo yao ya kazi.


Mhe. Kamwelwe amepongeza hatua ya uboreshaji wa sare hizo na kuwahimiza madereva na makondakta kuzivaa sare hizo wakiwa kazini na  kuzingatia usafi, unadhifu na matumizi ya lugha nzuri zinazojali abiria wakati wa utoaji huduma za usafiri.


Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Dar es Salaam, Leah Dotto amewashukuru viongozi wa DARCOBOA na UWADAR kwa kuendelea kuiamini VETA kufanya kazi ya kushona sare za madereva na makondakta wa dalalala ambapo kwa sasa wameweza kushona sare hizo mpya 6,000.


Amesema kupitia ushonaji wa sare hizo katika Chuo cha VETA Dar es Salaam, VETA imeweza kujenga nguvukazi iliyo tayari kuingia kwenye soko la ajira na kuanza kuzalisha moja kwa moja kwa kuwa wahitimu wa fani ya ushonaji hutumika pia kufanya kazi hiyo.

Dotto amemuhakikishia Waziri Kamwelwe kuwa VETA ina uwezo mkubwa wa kushona sare katika vyuo vyake vilivyosambaa nchi nzima na kuomba VETA iaminiwe kufanya kazi hiyo hata katika maeneo mengine kulingana na mahitaji. 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini – LATRA, Gilliad Ngewe amesema mabadiliko ya sare hizo yamelenga kuboresha muonekano wa madereva na makondakta wa jiji la Dar es Salaam.

Naye Mwenyekiti wa UWADAR, Kismat Jaffar amewasihi madereva na makondakta kutumia sare hizo mpya na kuwakikishia kuwa ubora wa sare hizo ni wa kiwango cha juu.



Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe (Mb), akizungumza wakati wa uzinduzi wa sare mpya za madereva na makondakta wa Daladala Mkoa wa Dar es Salaam.




Muonekano wa sare mpya za madereva na makondakta wa Daladala Mkoa wa Dar es Salaam. Sare hizo zimeshonwa na Chuo cha VETA Dar es Salaam.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe (Mb), akionyesha moja ya sare mpya za Madereva na Makondakta wa Daladala Mkoa wa Dar es Salaam, wakati wa uzinduzi wa sare hizo leo tarehe 6 Aprili, 2020. Sare hizo zimeshonwa na Chuo cha VETA Dar es Salaam.



No comments:

Post a Comment