CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Wednesday 11 April 2018

Mafunzo ya ufundi stadi yawahamasisha viziwi kufungua mgahawa


Mafunzo ya mapishi na mapambo yaliyotolewa kwa vijana wilayani Kilombero, mkoani Morogoro kupitia chuo cha VETA Mikumi, yamewasaidia vijana viziwi kujenga ujasiri, hivyo kufungua mgahawa wa chakula unaotoa huduma katika mji wa Ifakara.

Mafunzo hayo yaliyotolewa chini ya mradi wa Uwezeshaji Vijana Kiuchumi (YEE) katika kipindi cha kati ya mwaka 2015 hadi mwaka 2018 yalilenga katika kuwapatia vijana, hususani wa makundi maalum mafunzo ya ufundi stadi ili kuwawezesha kujikwamua kiuchumi kwa kujiajiri au kuajiriwa.

Ulemavu wa kutosikia haujawazuia Bi. Elizabeth Lutta na Mwatanga Kibwana kutumia ujuzi walioupata katika mafunzo hayo kwa kuanzisha mradi wa mgahawa wa kwao wenyewe.

Mgahawa huo walioupa jina la EMFRANJO Catering and Decoration upo katikati ya mji wa Ifakara na unavutia wengi kutokana na uwezo wanaoonyesha viziwi hao katika mapishi na ukarimu wao katika kuhudumia wateja.

 Pamoja na ulemavu walio nao, wameendelea kupambana na ushindani wa kibiashara, jambo ambalo linashangaza wengi, hasa juu ya namna ambavyo wanaweza kuwasiliana na kuelewana na wateja wao na kuwafanya kufurahia na kuridhika na huduma zao.

 Bi Lutta anasema mwanzoni ilikuwa tabu sana wateja kuelewana nao kwa kuwa wao wanatumia lugha ya alama ambayo watu wengi hawaifahamu, lakini walimudu changamoto hiyo kwa kutumia njia mbalimbali na kwa sasa watu wengi wanaofika kupata huduma wanafahamu kuwa hawasikii na hivyo hutumia mbinu mbalimbali kuwasiliana nao, ikiwemo kuandika au kuonesha picha za huduma wanazohitaji.

“Ilikuwa ngumu watu kuamini kuwa wanaweza kuhudumiwa na watu wenye changamoto ya usikivu kama sisi, lakini baada ya muda watu wametuamini na wanakuja kupata huduma kwetu kwa kuwa tunajitahidi kupika chakula kizuri na kuonesha huduma bora kwa wateja wetu”Anasema

Kwa upande wake Bi. Mwatanga Kibwana anasema baada ya kuanza biashara hiyo kwenye kikundi anaweza kumudu mahitaji yake na kuchangia mahitaji ya familia yake tofauti na ilivyokuwa mwanzoni kabla ya kupata mafunzo.

Anasema wanaiona biashara yao ikiendelea kwa mafanikio kwani wanaaminika na wameanza kupata zabuni za kuhudumia katika vikao mbalimbali hasa vya serikali za kata, halmashauri na vyama.

Meneja wa Mradi wa YEE Ifakara Bw Majani Rwambali anasema mradi huo umeonesha mafanikio makubwa kwa kuwafikia  na kuwapatia mafunzo ya ufundi stadi jumla ya vijana 1470 wa wilaya hiyo ambapo wengi wao wameweza kujiajiri na wengine wameajiriwa.

Mafunzo hayo yalihusisha fani za ushonaji, useremala, ujenzi, uchomeleaji, mapishi na mapambo, ufundi simu, umeme, pamoja na udereva na ufundi wa magari.

Mradi wa YEE ulianza mwaka 2015 kwa ufadhili wa Jumuiya ya Ulaya na unatekelezwa kwa ushirkiano kati ya VETA, Plan International na asasi za CODERT na UHIKI.

No comments:

Post a Comment