CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 8 November 2018

IMTT Kuwa Mpango wa kudumu wa mafunzo ukihusisha sekta mbalimbali




Wadau wa Mradi wa Mafunzo Jumuishi ya Ujuzi kwa Ajili ya Sekta ya Madini (Integrated Mining Technical Training-IMTT) wamekubaliana kuukuza na kuupanua mradi huo ili uwe Mpango maalum wa mafunzo utakaohusisha sekta na wadau mbalimbali zaidi ya makampuni ya madini. Mradi huo unaoendeshwa kwa mfumo wa uanagenzi kupitia chuo cha VETA Moshi uliasisiwa na makampuni ya uchimbaji madini kupitia Chemba ya Nishati na Madini Tanzania(TCME) kwa ushirikiano na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA).


Wazo la kubadili mradi huo kuwa mpango maalum lilijadiliwa na kuafikiwa tarehe 2 Novemba, 2018 katika kikao cha pamoja cha Kamati ya Uwakilishi katika Usimamizi wa Mradi (Representative Management Committee-RMC) inayoundwa na  wadau wa mradi huo ambao ni pamoja na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA); Chemba ya Nishati na Madini Tanzania(TCME); Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia; na Wawakilishi wa Makampuni ya Madini.


Katika kikao hicho kilichafanyika kwenye chuo cha VETA Moshi chini ya Uwenyekiti wa Janet Reuben kutoka TCME, wadau walijadili na kuzingatia ukweli kuwa tangu kuanzishwa kwake mwaka 2008, mradi huo umezidi kukua na kupanuka katika katika utoaji wa mafunzo huku makampuni zaidi hata yale ya yasiyohusika na madini yakizidi kujiunga, hivyo tafsiri kuwa mradi huo ni maalum kwa mafunzo kwa ajili ya kusaidia sekta ya madini pekee kuzidi kufifia.

Wadau hao walikubaliana kuwa hata jina libadilike na kuwa Mpango wa Mafunzo Jumuishi ya Ufundi (Integrated Technical Training Programme-ITTP).


“kwa kweli mradi umepanuka sana na wadau wengi wamejiunga na wengine wanaendelea kuonesha nia ya kujiunga kutoka sekta mbalimbali. Kwa hiyo hata uhalali wa kuendelea na jina la awali la IMTT unaanza kukosekana,” alisema Shayo Simon, Makamu wa Rais anayehusika na Uendelevu kutoka kampuni ya Geita Gold Mining Tanzania-GGM.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu licha ya kuwashukuru wadau kuendelea kusaidia vijana kupata mafunzo kupitia mradi huo, alisema kuwa VETA iko tayari kuendelea na mafunzo hayo katika utaratibu wa kuwa na Mpango mmoja ambamo makampuni na wadau kutoka sekta mbalimbali watakuwa wakiingia na miradi ya vipindi tofauti tofauti.



Akiwasilisha taarifa ya maendeleo ya IMTT, Mratibu wa Mradi huo Theresia Mosha alisema kuwa katika kipindi cha kuanzia mwaka 2009 hadi 2018 mradi ulidahili jumla ya wanagenzi 825 katika fani mbalimbali ambapo 448 walihitimu, 265 wakiwa bado wako mafunzoni na 112 waliacha mafunzo. 


Mradi wa IMTT ulianzishwa mwaka 2008 kwa ushirikiano kati ya VETA na TCME kwa madhumuni ya kutoa mafunzo bora kwa ajili ya kusaidia sekta ya madini; kuzalisha mafundi stadi mahiri watakaochangia maendeleo na ukuaji wa uchumi wa Tanzania; kukuza mahusiano baina ya vyuo na waajiri  kama migodi na sekta nyingine pamoja na Kutoa mafundi wenye  utaalamu unaoendana na teknolojia ya kisasa. Mafunzo hayo huendeshwa kwa mfumo wa uanagenzi ambao unahusisha mafunzo kwa kupokezana kati ya chuo na mahala pa kazi katika mzunguko kipindi chao chote cha mafunzo.

Kozi ambazo zimekuwa zikitolewa kupitia mradi huo ni pamoja na Umeme wa Magari; Ufundi wa Mashine na Mitambo Mikubwa; Umeme wa Majumbani; Utengenezaji wa Vipuli kwa ajili ya Mitambo na Mashine; na Uungaji Vyuma. Kozi zingine ni pamoja na Ubebaji wa vitu vizito; Udereva; Kompyuta na Mfumo wa Mafuta na Upepo (Hydraulic and Pneumatic). Makampuni washirika wa mradi huo ni pamoja na ACACIA (Bulyanhulu; Buzwagi, North Mara); Geita Gold Mining; Kabanga; Sandvik; Mantrac; Pan-Africa; Atlass copco na Shanta Gold Mine.

No comments:

Post a Comment