CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 8 November 2018

VETA Kagera kuanzisha mafunzo ya Ufugaji, Uandaaji na Uhifadhi wa samaki


Chuo cha Ufundi Stadi Kagera (VETA Kagera) kina mpango wa kuanzisha mafunzo ya Ufugaji, Uandaaji na Uhifadhi wa samaki ili kwenda sambamba na mazingira na shughuli za kiuchumi zinazoendeshwa na wakazi wanaokizunguka chuo hicho pamoja na mkoa wa Kagera na mikoa ya kanda ya Ziwa kwa ujumla.

Mkuu wa Chuo cha VETA Kagera, Baluhi Mitinje aliyabainisha hayo hivi karibuni wakati wa ziara ya Menejimenti ya VETA katika chuo hicho.

Alisema sehemu kubwa ya Mkoa wa Kagera iko kandokando au imezungukwa na Ziwa Victoria na shughuli nyingi za uvuvi zinafanyika katika mkoa huo, hivyo chuo chake kimeona ipo fursa na haja ya kujengea ujuzi wakazi wa Kagera na mikoa ya jirani katika ufugaji na usindikaji wa samaki.

Alisema, ujuzi utakaofundishwa ni wa ufugaji kwa kutumia vizimba-cages na kuandaa na kuhifadhi samaki kwa njia ya kubanika kwa kutumia matanuru ya kisasa.

“Ukiangalia eneo kubwa la Kagera limezungukwa na ziwa na shughuli za wananchi zinahusiana na uvuvi, kwa hiyo tumeona tuitumie fursa hii kwa kuwapa ujuzi ili waweze kuboresha shughuli zao,” alisema.

Alisema mafunzo hayo yanatarajiwa kuanzishwa kwa ufadhili wa Mfuko wa Uendelezaji Ujuzi (Skills Development Fund-SDF) unaoratibiwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) ambapo VETA Kagera iliandaa andiko na kufanikiwa kupata fedha za mradi wa kuanzisha mafunzo hayo.

Sambamba na mafunzo yanayohusiana na samaki, Mitinje aliongeza kuwa chuo hicho pia kinapanga kuanzisha mafunzo ya muda mfupi katika ujuzi wa Ususi na Urembo (Cosmetology); Umeme wa Jua (Solar); Utengenezaji wa Mashine za Ofisi; Ukarimu kwa Wageni (Hospitality);  Ufundi Bomba (Plumbing); na kuimarisha zaidi mafunzo ya udereva wa magari.

Chuo cha Ufundi Stadi Kagera (VETA Kagera) kilianzishwa mwaka 1987 chini ya Idara ya Mafunzo na Majaribio ya Idara ya Ufundi iliyokuwa ndani Wizara ya Kazi na Ustawi wa Jamii. Chuo kilianza kwa uwezo wa kudahili wanafunzi 120 kwa mwaka kwa fani nne ambazo ni Useremala, Uashi, Ushonaji wa Nguo na Uungaji Vyuma.

Sasa chuo hicho kimefikia uwezo wa kudahili wanafunzi zaidi ya 300 katika fani za muda mrefu na zaidi ya wanafunzi 800 kwa kozi za muda mfupi kwa mwaka katika fani sita za Ufundi wa Magari, Umeme,  Useremala, Uashi, Ushonaji wa Nguo na Uungaji Vyuma.
 

No comments:

Post a Comment