CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 8 November 2018

Mkurugenzi Mkuu VETA ahimiza ubunifu katika ufundi stadi

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt Pancras Bujulu amewahimiza walimu wa ufundi stadi kuweka mkazo katika ujuzi na ubunifu kwenye utoaji wa mafunzo ili kuwezesha kutoa wahitimu mahiri na wabunifu, hivyo kuonesha thamani ya mafunzo yatolewayo chuoni na kuvutia vijana wengi zaidi kujiunga na elimu na mafunzo ya ufundi stadi.  

Akizungumza na walimu na wafanyakazi wa chuo cha VETA Kagera, Oktoba 29, 2018 baada ya kufanya ziara katika chuo hicho, Dkt Bujulu aliwaasa walimu kuwiwa zaidi kutoa ujuzi na maarifa waliyonayo kwa wanafunzi na kusema kuwa ujuzi katika fani ni suala la msingi zaidi kuliko hata juhudi za kumuwezesha mwanafunzi kufaulu mtihani, kwani ujuzi ndio utakaowawezesha wanafunzi kutenda kazi baada ya kuhitimu.

 “Kufaulu mtihani ni ishara ya ujuzi, lakini haitoshi maana inategemea siku ile uliamkaje, mtihani ulitungwaje, ilitungwa mada ipi ambayo ulijiandaa kuliko nyingine, lakini ujuzi ulioupata ni wa msingi zaidi kwa kuwa unakwenda kuufanyia kazi kuliko mtihani uliofaulu,” alisema.

Alisema mwanafunzi aliyepo chuoni akipewa ujuzi bora, maarifa na mwanga zaidi wa kuweza kupambanua mambo kutamwezesha kuwa mbunifu pia na kumtofautisha na yule aliyejifunza kupitia mfumo usio rasmi.

Alifafanua kuwa hata fani ambazo udahili wake ulionekana uko katika kiwango cha chini unaweza kuongezeka iwapo watu watabaini kuwa mafunzo chuoni ni bora zaidi kuliko yale ya mtaani.

Aliongeza kuwa kuna watu wenye mtazamo kwamba baadhi ya fani hazihitaji kwenda chuoni kujifunza, kwani unaweza kujifunza mtaani na kuwa na ujuzi sawa tu na aliyekwenda chuoni na kusema kuwa mtazamo huo unaweza kuondolewa kwa mhitimu wa chuo cha ufundi stadi kuonesha umahiri, ubunifu na uwezo wa kupambanua mambo kwa undani zaidi kuliko aliyejifunz mtaani.

Akielezea maendeleo ya chuo cha VETA Kagera, Mkuu wa Chuo hicho Baluhi Mitinje alisema licha ya chuo hicho kufanikiwa kuongeza udahili hadi kufikia wanafunzi 302 katika daraja la 1, la 2 na la 3, baadhi ya fani ikiwemo ushonaji na useremala zimekuwa na mwitikio mdogo wa vijana kujiunga nazo.

Alisema fani hizo zinakosa sifa ya kupendwa na vijana na akatoa mfano wa takwimu za  mwaka 2018 ambapo fani ya Ushonaji imedahili jumla ya wanafunzi 21 tu katika ngazi zote za 1, 2 na 3 huku Useremala nako wakidahiliwa jumla ya wanafunzi 23 tu katika ngazi zote tatu.

Chuo cha Ufundi Stadi Kagera ni miongoni mwa vyuo vitatu vinavyomilikiwa na VETA vilivyopo Kanda ya Ziwa, ambacho kwa sasa kinatoa mafunzo katika fani za Ufundi Magari, Umeme, Useremala, Uashi, Ushonaji nguo na Uungaji vyuma.

No comments:

Post a Comment