CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 22 November 2018

Wasomi vyuo vikuu watakiwa kujifunza ufundi stadi



Wasomi wa vyuo vikuu nchini wameshauriwa kujifunza ufundi stadi ili kujiongezea ujuzi na ubunifu utakaowawezesha kujiajiri.

Ushauri huo umetolewa na Mwenyekiti wa Baraza la Chuo cha Walimu wa Ufundi Stadi Morogoro (MVTTC), Profesa  Elifas Bisanda wakati wa uzinduzi wa Baraza hilo tarehe 15 Novemba 2018.

Profesa Bisanda, ambaye pia ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria amesema ni vyema wasomi nchini wakaondokana na dhana ya kuwa usomi ni kuajiriwa katika maofisi na badala yake watumie usomi wao katika kujiongezea ujuzi wa ufundi stadi ambao wanaweza kuutumia kubuni miradi na huduma ambazo zitasaidia kutatua changamoto mbalimbali katika jamii huku zikiwanufaisha wao kwa kipato.

Amesema kwa kuzingatia mkakati na mwelekeo wa nchi kwenye uchumi wa viwanda miongoni mwa mikakati ya VETA itakuwa ni kuwahamasisha vijana hao wasomi wanaomaliza vyuo vikuu ambao wanatafuta ajira kuingia kwenye mafunzo ya ufundi stadi ili wawe na uwezo wa kubuni vitu mbalimbali hata kama wamesomea kozi nyingine.

Amesema wahitimu wa vyuo vikuu wakiongezea maarifa yao na ujuzi kutoka vyuo vya ufundi stadi itakuwa rahisi kujiajiri  na kufikia malengo yao.

Profesa Bisanda alitoa mfano wa nchi ya Korea ambapo wahitimu wengi wa vyuo vikuu katika nchi hiyo ndio wanaojiunga na vyuo vya ufundi na kwamba asilimia 95 ya wanafunzi wanaojiandikisha darasa la kwanza kwa nchi hiyo wanamaliza elimu cha chuo kikuu tofauti na hapa nchini ambapo ni asilimia 4 pekee ndio wanaofika ngazi ya chuo kikuu.

“Nchi ya Korea huwezi kuwa mwalimu bila kuwa na degree na ndio wanaoenda vyuo vya ufundi, lakini huku kwetu wanaofeli darasa la saba ndio wanaojiunga na vyuo vya ufundi stadi. Ifikie mahali mifumo yetu ya Tanzania ibadilike ili kuhakikisha tunapata ufanisi na ujuzi kwa watoto wetu,”alisema Profesa Bisanda

Akizungumza na wajumbe wa Baraza hilo la Chuo cha ualimu na ufundi stadi (MVTTC)Morogoro Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro Lukas Mwaisaka kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dk Steven Kebwe, amewakumbusha jukumu lao katika kusimamia vyema chuo hicho maalum kwa ajili ya walimu wa ufundi stadi, ili kiweze kutoa walimu bora watakaohamisha ujuzi wao kwa wanafunzi wa ufundi stadi katika vyuo mbalimbali nchini.

Amesema jukumu la MVTTC ni kubwa kwa kuwa ni chuo pekee cha mafunzo ya Walimu wa Ufundi Stadi nchini huku vyuo vya ufundi stadi vikiwa ni 550 sasa na bado kuna vingine vinatarajiwa kuanzishwa muda si mrefu.  

Amesema kuwa matumaini ya Serikali ni kuona chuo hicho pamoja na kutoa mafunzo kwa waalimu wa ufundi stadi pia  kinatoa mafunzo kwa viongozi wa vyuo vya ufundi stadi ili wawe na sifa pekee za kusimamia utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu aliwaagiza watendaji wa MVTTC kufikiria kuandaa walimu wenye stadi za kufundisha watu wenye ulemavu kwa kuwa sasa VETA inakabiliwa na changamoto za ufundishaji ufundi stadi kwa watu wenye ulemavu.

Aliwaomba wajumbe wa Baraza la MVTTC kukishauri chuo hicho na kuhimiza kuanzisha mipango na mikakati mbalimbali ya kuanza kuandaa walimu wa ufundi stadi katika mwelekeo wa kufundisha watu wenye uemavu.




No comments:

Post a Comment