CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Wednesday 10 April 2019

Timu toka Afrika Kusini yavutiwa na namna VETA inavyorasimisha ujuzi


Timu ya wataalam kutoka Afrika Kusini imevutiwa na namna Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) inavyotekeleza mpango wa Urasimishaji Ujuzi uliopatikana nje ya Mfumo Rasmi wa Mafunzo (RPL) na kuahidi kujipanga kwa ajili ya kuanzisha ushirikiano na VETA katika eneo hilo.

Wajumbe wa timu ya Wakala wa Taifa wa Maendeleo ya Vijana nchini Africa Kusini (NYDA) walibainisha hayo baada ya kupata maelezo ya utekelezaji wa mpango huo nchini wakati wa kikao chao na Menejimenti ya VETA walipotembelea Makao Makuu ya VETA jijini Dar es Salaam, tarehe 2 Aprili 2019 wakati wa ziara yao iliyokuwa chini ya uenyeji na uratibu wa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC).

Mkurugenzi Mtendaji wa NYDA, Ankie Motsoahae alisema kuwa wamevutiwa sana na maelezo ya namna VETA inavyoendesha mpango wa RPL na kusema kuwa ingawa nchini Afrika kusini kuna mpango kama huo, lakini utekelezaji haujafanyika kwa kipindi kirefu, hivyo mpango umebaki kwenye nyaraka pekee. 

“Kwangu mimi RPL ni jambo la kuondoka nalo. Kama sehemu ya ushirikiano wetu na Tanzania, tungependa kupata uzoefu kuhusiana na RPL. Tunatarajia kuja tena ndani ya miezi miwili ili kurasimisha ushirikiano katika maeneo mbalimbali.” Alisema.

NYDA ina majukumu ya kuendeleza vijana nchini Afrika Kusini na elimu ni miongoni mwa sekta za kipaumbele katika kuwaendeleza vijana.  Timu hiyo ya NYDA ilifika nchini kwa ajili ya kubainisha maeneo ya ushirikiano katika nyanja mbalimbali ikiwemo elimu na ilitembelea baadhi ya taasisi nchini zikiwemo VETA; Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH); Baraza la Michezo Tanzania (BMT); Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA); Wakala wa Huduma za Ajira (TaESA); Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TASUBA); Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na Chuo Kikuu cha Mzumbe. 




1 comment:

  1. Niapongeza VETA kwa kujiimarisha katika kupanua mpango huu wa urasimishaji wa ujuzi uliopatikan nje ya mfumo rasmi wa mafunzo. ILO itaendelea kushirikiana na nyi katika kuboresha viwango na utaalam katika eneo hili.

    ReplyDelete