CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 20 May 2019

VETA na Swisscontact zaingia makubaliano kuimarisha mfumo wa upatikanaji wa taarifa za soko la ajira


Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imeingia  makubaliano na Shirika la Kimataifa la Swisscontact kwa lengo la kuboresha mfumo wa upatikanaji wa taarifa za soko la ajira ili kuimarisha utoaji mafunzo ya ufundi stadi. 

Makubaliano ya mradi huo uliopewa jina la Ujuzi kwa Ajili ya Ajira (Skills for Employment Tanzania) yamesainiwa leo Mei 14, 2019 katika ofisi za VETA Makao Makuu kati ya Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu, na Msimamizi wa Mradi wa Swisscontact, Ndg. Soren Poulsen.

Akizungumza wakati wa kusaini makubaliano hayo, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu, amesema mradi huo utasaidia kuongeza fursa za ajira kwa vijana wanaohitimu mafunzo ya Ufundi stadi kupitia upatikanaji wa taarifa sahihi za mahitaji ya soko zitakazosaidia kuhuisha mitaala ya utoaji mafunzo.

“Tunatambua umuhimu wa taarifa za soko la ajira katika kuboresha utoaji mafunzo na kuzalisha nguvu kazi inayohitajika na soko la ajira ndiyo maana tunaona kuwa mradi huu utakuwa wa manufaa kwetu.” Alisema

Naye Msimamizi wa Mradi wa Swisscontact Ndg. Soren Poulsen, alisema kuwa anaamini kuwa mradi huo utatoa mchango mkubwa katika kuboresha mchakato wa ukusanyaji taarifa za soko la ajira na kuimarisha mahusiano kati ya watoa mafunzo na waajiri nchini.

Alitaja maeneo ambayo yatapewa kipaumbele kupitia mradi huo kuwa ni pamoja na kuwajengea uwezo wakusanya taarifa wa Mamlaka (Labour Market Analysts), kuboresha mbinu za ukusanyaji taarifa, kuongeza ushiriki wa waajiri katika utoaji taarifa za mahitaji yao ili kusaidia ukuzaji wa mitaala na kukiongezea uwezo Chuo cha Ualimu wa Ufundi Stadi Morogoro (MVTTC) katika utoaji na usimamizi wa mafunzo.

Makubaliano hayo yatadumu kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia 2019 hadi 2022 na muda utaweza kuongezeka kulingana na makubaliano ya pande zote mbili.


No comments:

Post a Comment