CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 20 May 2019

Wahasibu wakumbushwa kuzingatia maslahi ya umma


Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA), Pius Maneno amewakumbusha Wahasibu kuzingatia maslahi ya umma kwani ndio matakwa ya msingi ya taaluma ya Uhasibu.

Akifungua mafunzo ya Viwango vya Kimataifa vya Uandaaji wa Mahesabu ya Sekta za Umma (International Public Sector Accounting Standards) kwa watumishi wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), kwenye Chuo cha VETA Dodoma, leo tarehe 20 Mei, 2019, Maneno alisema tofauti na baadhi ya taaluma ambazo wakati mwingine mhusika hutazama maslahi binafsi, taaluma ya Uhasibu daima ni ya kuzingatia maslahi ya umma.

“ndio maana hata kaulimbiu ya Bodi yetu ni Msemakweli. Sisi si watu wa kupindisha pindisha kwa maslahi ya mtu binafsi, mara zote tunazingatia maslahi ya umma na kusema ukweli,” alisema.

Sambamba na hilo, Maneno aliwaomba Wahasibu wa VETA kuhakikisha mahesabu ya taasisi yanapangwa vyema kwa kuzingatia viwango vya uhasibu na kuialika VETA kuingia katika mashindano ya Upangaji Bora wa Mahesabu ambayo NBAA imeyaanzisha.

“unaweza kupata hati safi ya ukaguzi wa hesabu zako, lakini mahesabu yako yakawa hayajapangwa vizuri, ndio maana NBAA tumeanzisha mashindano hayo na nawaomba VETA muingie kwenye kinyang’anyiro hicho,” alisema.

Aliongeza kuwa NBAA inafikiria kupunguza muda wa uandaaji na uwasilishaji wa taarifa za ukaguzi wa hesabu, kwani muda wa miezi sita wa sasa ni mrefu mno na endapo kwenye taarifa kuna dosari zinazohitaji marekebisho, mhusika anaweza asipate muda wa kutosha kuzirekebisha kabla ya mwaka mpya wa fedha.

Akitoa neno, Kaimu Mkurugenzi wa Fedha wa VETA, Anthony Kasore alisema VETA imekuwa ikizingatia viwango, misingi na taratibu za uandaaji wa mahesabu na kwamba kumekuwa na ushirikiano wa karibu miongoni mwa wahasibu kutoka kanda na vituo mbalimbali vya VETA katika kuandaa mahesabu na kuhakikisha yanakaguliwa kwa wakati.

Alisema, ili kuhakikisha kuwa wahasibu wa VETA wanaendelea kuongeza maarifa na kukidhi viwango na vigezo vya taaluma, Mamlaka imekuwa ikiandaa mafunzo na semina mbalimbali za kuwajengea uwezo na kuwaimarisha.



No comments:

Post a Comment